VYAMA 99% VYASAINI KANUNI ZA MAADILI YA UCHAGUZI 2025 – INEEC YAONYA WASIOSAINI

 

   


      📌BAHATI MSANJILA


Asilimia 99 ya vyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu nchini vimesaini Kanuni za Maadili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, huku Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEEC) ikionya kuwa vyama ambavyo havijasaini kanuni hizo vitazuiwa kushiriki uchaguzi huo.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa kanuni hizo, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji wa Rufani Jacob Mwambegele, amesema kuwa mchakato wa kuandaa kanuni hizo umezingatia maoni ya wadau mbalimbali, wakiwemo wawakilishi wa vyama vya siasa.

“Kila chama cha siasa kinapaswa kusaini kanuni hizi. Chama chochote kitakachoshindwa kufanya hivyo, hakitaruhusiwa kushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa 2025,” amesema Jaji Mwambegele.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uchaguzi na Katibu wa Tume hiyo, Ramadhani Kailima, amesema kuwa zoezi la kusaini kanuni hizo ni sehemu ya utekelezaji wa matakwa ya sheria mpya za uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, zenye lengo la kudhibiti matumizi ya lugha chafu na vitendo vinavyoweza kuvuruga uchaguzi.

Baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa walioshiriki hafla hiyo wamesema wamesaini kanuni hizo kwa kuwa ni hitaji la kisheria, na wamepongeza ushirikishwaji waliopata tangu hatua za awali za uandaaji wa kanuni hizo, hadi hatua ya mwisho ya utiaji saini.

Miongoni mwa vyama vilivyosaini kanuni hizo ni pamoja na AAFP, ACT Wazalendo, ADA-TADEA, CCK, CHAUMA, CCM, CUF, ADC, TLP, UDP, Demokrasia Makini, DP, SAU, NCCR Mageuzi, UMD, NLD, UPDP, na NRA.

Hata hivyo, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) hakikushiriki katika zoezi hilo la utiaji saini wa Kanuni za Maadili ya Uchaguzi.










Post a Comment

0 Comments