SERIKALI YAMALIZA TATHMINI YA ATHARI ZA KUPUNGUA KWA UFADHILI WA MAREKANI, SEKTA YA AFYA YAATHIRIKA ZAIDI – DKT. MWIGULU

 




      

  📌BAHATI MSANJILA

Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imekamilisha tathmini ya awali ya athari zitakazojitokeza kwenye miradi iliyokuwa ikifadhiliwa na Serikali ya Marekani, ambapo sekta ya afya imeonekana kuathirika zaidi.

Dkt. Nchemba ametoa kauli hiyo leo, Aprili 15, 2025, bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum (Kagera), Neema Lugangira, aliyehoji hatua zinazochukuliwa na Serikali kupunguza athari za mabadiliko ya sera za nje katika masuala ya fedha za maendeleo kutoka kwa nchi zilizoendelea.

Aidha, Waziri huyo aliongeza kuwa Serikali inaendelea kufanya tathmini katika maeneo mengine ambayo huenda yakaathirika kwa kiasi kikubwa kutokana na mabadiliko hayo ya sera, huku ikizingatia mchango wa mashirika na wahisani wengine wa maendeleo ambao awali waliwezeshwa na Marekani.

Katika swali la nyongeza, Mbunge Lugangira alihoji iwapo Serikali haioni haja ya kuondoa matumizi yasiyo ya lazima ili kuokoa fedha ambazo zinaweza kuelekezwa kufidia upungufu wa ufadhili huo.

Akijibu, Dkt. Nchemba alisema tayari Serikali imeanza kuchukua hatua, ikiwemo kuunda timu maalum chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambayo ilifanya mapitio ya sekta zote, na kubaini kuwa sekta ya afya ndiyo inayohitaji msaada wa haraka zaidi.




Post a Comment

0 Comments