Waziri wa
Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry Silaa (Mb), amesema Serikali
kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) inatekeleza ujenzi wa minara 38
ya mawasiliano mkoani Kilimanjaro kwa gharama ya shilingi bilioni 7.1, ikiwa ni
sehemu ya juhudi za kuhakikisha huduma bora za mawasiliano zinafika maeneo ya
vijijini.
Akiwa katika ziara
ya kukagua upatikanaji wa huduma hizo wilayani Mwanga, Waziri Silaa alizungumza
na wananchi wa Kijiji cha Karamba Ndea, Kata ya Toloha, na kueleza kuwa kati ya
minara hiyo, sita inajengwa katika wilaya ya Mwanga, ikiwemo mnara unaohudumia
eneo la lango la kuingilia na kutoka watalii la Ndea kwenye Hifadhi ya Taifa ya
Mkomazi.
“Minara hii
itasaidia kutatua changamoto ya ukosefu wa mawasiliano ya simu kwa wananchi na
pia katika maeneo muhimu ya kitalii kama lango la Ndea,” alisema Mhe. Silaa.
Aidha, Waziri Silaa alieleza kuwa Serikali imekamilisha mradi wa
kuboresha teknolojia ya mawasiliano kwa kuhuisha minara 468 nchini kutoka
teknolojia ya kizazi cha pili (2G) kwenda teknolojia ya kizazi cha tatu (3G) na
cha nne (4G), ili kuwawezesha wananchi kupata huduma za intaneti kwa ufanisi
zaidi.
Katika kukabiliana
na changamoto za mawasiliano kwenye lango la Ndea na maeneo mengine, Waziri
aliielekeza UCSAF kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) pamoja
na watoa huduma kuhakikisha ujenzi wa minara unatekelezwa haraka. Pia
alisisitiza kuwa maeneo yote yenye changamoto ya mawasiliano yaliyoripotiwa na
viongozi wa eneo hilo, yatatupiwa jicho kwa ufumbuzi wa haraka.
Mkuu wa Wilaya ya
Mwanga, Mhe. Mwanahamisi Munkunda, alisema kuwa uwepo wa huduma bora za
mawasiliano utachochea shughuli za maendeleo, kukuza sekta ya utalii, na kuimarisha
uchumi wa kidigitali katika wilaya hiyo.
Kwa upande wake,
Diwani wa Kata ya Toloha, Mhe. Palesio Nalio, alishukuru Serikali kwa mradi huo
na kusisitiza umuhimu wa kukamilisha miradi ya kuboresha usikivu wa redio,
kwani baadhi ya wananchi wamelazimika kusikiliza redio za nchi jirani kutokana
na ukosefu wa mawimbi ya redio za ndani.
Serikali kupitia
UCSAF inatekeleza mradi wa kimkakati wa ujenzi wa minara 758 katika kata 713
zilizopo kwenye mikoa yote ya Tanzania Bara. Kwa Mkoa wa Kilimanjaro, minara 38
imepangwa kujengwa ambapo hadi kufikia tarehe 9 Aprili 2025, jumla ya minara 20
ilikuwa tayari imeanza kutoa huduma.
Katika Wilaya ya
Mwanga, minara 6 imepangwa kujengwa ambapo mitatu tayari imekamilika na ipo
kazini, huku mingine mitatu ikiwa kwenye hatua mbalimbali za ujenzi. Kwa
ujumla, ujenzi wa minara yote 18 iliyosalia mkoani humo unaendelea kwa kasi.
0 Comments