UCSAF YATOA VIFAA VYA TEHAMA KWA SHULE ZA UMMA ILI KUBORESHA MAZINGIRA YA KUJIFUNZA

 

   


📌Na Mwandishi Wetu,

Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umetoaa vifaa vya TEHAMA kwa shule za umma 1,121 ikiwemo kompyuta, projekta na printa ili kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi wanaosoma shule mbalimbali za umma nchini.

Hayo yameelezwa leo jijini Dodoma na Afisa Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Mhandisi Peter Mwasalyanda wakati akizungumza na Waandishi wa habari kuhusu mafanikio na mwelekeo wa Mfuko huo kwa Kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt, Samia Suluhu Hassan.

Mhandisi Mwasalyanda amesema, sambamba na utekelezaji wa mradi huo, UCSAF imekuwa ikiratibu mafunzo ya TEHAMA kwa shule ambazo zinafikishiwa vifaa hivyo ili kuwawezesha walimu kuvilewa vifaa hivyo na kutatua matatizo madogo madogo pindi vinapopata matatizo.

Kwa mujibu wa Mhandisi Mwasalyanda, katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, UCSAF imefanikiwa kutoa mafunzo kwa walimu 3,798 kutoka shule 1,791 za umma nchini, kwa kushirikiana na vyuo vikuu na taasisi za elimu nchini, ikiwemo Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

Kwa upande mwingine, Mhandisi Mwasalyanda amesema UCSAF imeendelea kuhamasisha matumizi ya TEHAMA kwa wasichana, kupitia maadhimisho ya Siku ya Wasichana na TEHAMA, ambapo mafunzo yanatolewa kwa wanafunzi wa kike ili kuwaandaa kwa masomo ya sayansi na teknolojia.

Katika kipindi cha Awamu ya sita chini ya Mhe. Rais Dr. Samia Suluhu Hassan, UCSAF imetoa mafunzo kwa wanafunzi takribani 490 kutoka shule 304. Kwa mwaka wa Fedha 2024/25 wanafunzi wa kike wapatao 248 wanatarajiwa kuhudhuria mafunzo haya.

Utekelezaji huu wa UCSAF ni sehemu ya juhudi za Serikali katika kuboresha elimu nchini, huku ikiendelea kutoa kipaumbele kwa maeneo ya TEHAMA na masomo ya sayansi na teknolojia, ili kuendana na mabadiliko ya haraka ya kiteknolojia duniani.





Post a Comment

0 Comments