SERIKALI YAJENGA MAABARA YA KISASA KUBORESHA SEKTA YA MADINI

 




 ðŸ“ŒBAHATI MSANJILA

Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) imeanza ujenzi wa maabara ya kisasa jijini Dodoma kwa lengo la kuimarisha uchunguzi wa sampuli za madini na kuchochea ukuaji wa sekta hiyo.

Ujenzi huu ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuboresha sekta ya madini nchini.

Akizungumza na waandishi wa Habari Kaimu Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi wa Huduma za Maabara wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST), Notkka Banteze, amesema wanajenga maabara ya kisasa na Maabara hiyo itakuwa na vifaa vya kisasa vitakavyowezesha uchunguzi wa madini mbalimbali,

Ametaja uchunguzi wa madini utahusisha madini ya kimkakati kama vile kinywe (graphite), shaba, nickel, na madini tembo (heavy mineral sands).

Amesema Kwa mara ya kwanza, wachimbaji wadogo wataweza kupata huduma za uchunguzi wa sampuli kwa haraka zaidi, hivyo kupunguza gharama na muda wa kusubiri matokeo.

Ameongeza kuwa Katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, GST imeshuhudia ongezeko la bajeti kutoka shilingi bilioni 10 mwaka 2021/2022 hadi bilioni 110 mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 1,000.

Fedha hizi zimewezesha taasisi hiyo kuimarisha tafiti za madini, kuajiri wataalamu zaidi, na kununua vifaa vya kisasa kama mashine za mionzi za XRD na XRF kwa ajili ya uchunguzi wa sampuli za miamba na udongo.

Sambamba na ujenzi wa maabara, Serikali inatekeleza mradi wa kusogeza huduma za GST karibu na wachimbaji kwa kujenga ofisi na maabara mpya katika mikoa ya Geita na Mbeya. Maabara hizi zitawasaidia wachimbaji wadogo kufanya uchunguzi wa madini yao kwa uhakika zaidi na kuongeza tija katika shughuli zao.

Kwa upande wa tafiti za madini, GST imekamilisha utafiti wa jiolojia na jiokemia katika mikoa mbalimbali, ambapo matokeo yanaonesha uwepo wa madini ya dhahabu, urani, kaolin, chokaa, na metali adimu kama rare earth elements.

Pia, utafiti wa madini ya helium umefanyika katika mikoa ya Arusha, Manyara, Dodoma, Singida na Shinyanga, huku matokeo ya awali yakiashiria uwezekano wa hifadhi kubwa ya gesi hiyo muhimu kwa matumizi ya viwandani na tiba.

Katika kuboresha mifumo ya usimamizi wa sekta ya madini, Serikali inakamilisha ujenzi wa Kanzidata ya Taifa ya taarifa za madini, mfumo ambao utasaidia kuhifadhi na kusambaza taarifa muhimu kwa wawekezaji na wadau wa sekta hiyo. Hii ni hatua muhimu katika kuvutia uwekezaji na kuongeza mchango wa sekta ya madini kwenye pato la taifa.

Amesema Mafanikio hayo yamewezekana kutokana na uwekezaji mkubwa wa Serikali, usimamizi thabiti wa Wizara ya Madini, na jitihada za GST katika kuimarisha utendaji wake.




Post a Comment

0 Comments