SAFARI ZA MIZIGO KUPITIA SGR KUANZA MEI TRC YATHIBITISHA

 




📌BAHATI MSANJILA

 

Shirika la Reli Tanzania (TRC) linatarajia kuanza rasmi safari za mizigo kupitia Reli ya Kisasa (SGR) kati ya Mei na Juni mwaka huu, Hii ni baada ya kupokea mabehewa 264 kati ya 1,430 yaliyoagizwa kwa ajili ya kuboresha usafirishaji wa mizigo na kuimarisha uchumi wa taifa.

 

Akizungumza jijini Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa TRC, Masanja Kadogosa, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa maagizo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye amewekeza zaidi ya shilingi trilioni 30 katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya reli nchini.

 

Tangu kuanza kwa safari za abiria kupitia SGR kati ya Dar es Salaam na Dodoma, zaidi ya abiria milioni 2.1 wamesafiri, huku mapato ya shilingi bilioni 59 yakikusanywa. Kadogosa alieleza kuwa kwa sasa TRC inasafirisha abiria kati ya 6,000 hadi 7,000 kwa siku, hali inayoonyesha muitikio mkubwa kutoka kwa wananchi.

 

Aidha amesema serikali ipo katika mchakato wa kuanza ujenzi wa reli ya SGR Kanda ya Kusini, ambapo kwa sasa inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya mradi huo.

 

 Reli hiyo inatarajiwa kuunganisha Tanzania na nchi za Malawi na Msumbiji, hatua itakayoongeza fursa za biashara na usafirishaji wa mizigo katika ukanda huo.

 

Kadogosa amebainisha kuwa TRC imeagiza jumla ya mabehewa 1,430, ambapo mabehewa 264 tayari yamewasili na Kwa sasa, shirika linaendelea kukamilisha taratibu mbalimbali za kiutendaji ili kuhakikisha safari za mizigo zinaanza rasmi kati ya Mei na Juni mwaka huu.

 

Amesema kuwa treni ya mizigo kupitia SGR itakuwa na uwezo wa kubeba tani 120 kwa safari moja, kiwango ambacho ni mara tatu ya uwezo wa treni ya kawaida, jambo litakalorahisisha usafirishaji wa bidhaa ndani na nje ya nchi.

 

Kadogosa amefafanua kuwa mpango wa serikali ni kuendelea kupanua mtandao wa reli, ambapo ifikapo mwaka 2027, SGR inatarajiwa kufika Mwanza, na ifikapo mwaka 2028, itakuwa imefika Kigoma.

 

Aidha, serikali inaendelea na mkakati wa kuunganisha reli ya SGR hadi Burundi, hatua itakayowezesha Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji wa mizigo kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

 

Kuanzishwa kwa safari za mizigo kupitia SGR ni hatua muhimu kwa uchumi wa Tanzania, kwani kutapunguza gharama za usafirishaji wa bidhaa, kuongeza ufanisi wa biashara, na kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

 




Post a Comment

0 Comments