NMB NA JUMUIYA YA ALAT WAENDELEZA USTAWI WA DODOMA

 




📌BAHATI MSANJILA


Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ameishukuru Benki ya NMB na Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) kwa mchango wao katika kuendeleza maendeleo ya mkoa huo.

 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ametoa shukrani hizo wakati akizungumza kwenye hafla ya Iftar iliyoandaliwa na Benki ya NMB kwa wananchi wa mkoa wa Dodoma na wajumbe wa ALAT. 

 

Senyamule amesema uwepo wa ALAT jijini Dodoma kwa siku tatu ni fursa kubwa kwa wakazi na wafanyabiashara wa mkoa huo.

 

Amebainisha kuwa ziara ya viongozi wa ALAT katika miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa jijini Dodoma itawawezesha kueleza kwa Watanzania kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 

Kwa upande wake, Afisa wa Wateja Wakubwa na Serikali wa Benki ya NMB, Alfredy Shayo, amesema hadi mwishoni mwa mwaka 2024, benki hiyo imefanikiwa kufikia vijiji 1,000 kupitia kampeni ya NMB Kijiji Day. Kampeni hiyo inalenga kuunga mkono jitihada za serikali za kuhakikisha kila Mtanzania, popote alipo, anapata huduma za kifedha, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi wa taifa na mtu mmoja mmoja.

 

Shayo ameongeza kuwa kwa mwaka 2025, NMB inapanga kufikia wananchi 2,000 ili kuwawezesha kufungua akaunti ya NMB Pesa kwa gharama nafuu ya shilingi 1,000 pekee Akaunti hiyo inawapa wateja fursa ya kupata mikopo bila kulazimika kufika katika matawi ya benki.

 

Katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, Shayo amesema Benki ya NMB inatamani kutumia mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kuombea uchaguzi wa amani.

 

Aidha, ametoa wito kwa Jumuiya ya ALAT kushirikiana na NMB katika kutoa elimu ya kifedha kwa wananchi.

 

Kwa niaba ya wajumbe wa ALAT Mkoa wa Dodoma, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, White Zuberi, ameishukuru NMB kwa kuwaunganisha katika hafla ya Iftar, akisema hatua hiyo inaonesha umuhimu wa mshikamano na ushirikiano kati ya taasisi za kifedha na viongozi wa serikali za mitaa.

 

Zuberi amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewatia moyo kwa kutambua jitihada za baadhi ya halmashauri katika kuwahudumia wananchi kwa niaba ya Serikali Kuu. 

 

Amesema kutambuliwa huko kunawapa nguvu zaidi ya kuendelea kuwatumikia wananchi kwa uadilifu.

 

Akizungumza kwa niaba ya Shekhe wa Mkoa wa Dodoma, Shehe Ahmad Said, ameombea dua kwa Mwenyezi Mungu awabariki wote walioshiriki katika hafla ya Iftar na kuwajalia kila la kheri Watanzania wote pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.








Post a Comment

0 Comments