NIT KUKAMILISHA MAANDALIZI YA KOZI YA URUBANI, BILIONI 6 ZIWEKEZWA


 


   📌Na Mwandishi Wetu


Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kipo katika hatua za mwisho za maandalizi ya kuanza kutoa kozi ya urubani, ambapo Serikali imewekeza shilingi bilioni 6 kuhakikisha kozi hiyo inakidhi viwango vya kimataifa.

 

Mkuu wa chuo hicho, Dkt. Prosper Mgaya, amesema hayo wakati akizungumzia mafanikio ya NIT chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 

 Ameeleza kuwa chuo kinapaswa kupita hatua tano za kupata ithibati ya kimataifa, ambapo tayari nne zimekamilika, na hatua ya mwisho inahusisha kuthibitishwa rasmi kwa utoaji wa mafunzo hayo.

 

Kwa mujibu wa Dkt. Mgaya, Tanzania imekuwa ikitumia fedha nyingi za kigeni kuwasomesha marubani nje ya nchi, jambo linaloongeza gharama kwa wanafunzi na Serikali. 

 

Hata hivyo, kuanzishwa kwa kozi hiyo ndani ya NIT kutapunguza gharama za masomo kwa asilimia 50 hadi 60, hatua ambayo itawawezesha Watanzania wengi kupata mafunzo kwa urahisi zaidi.

 

Ameongeza kuwa programu hiyo itachangia kuongeza idadi ya marubani wazawa na kupunguza utegemezi wa marubani wa kigeni ambao hulipwa gharama kubwa.

 

Pia, itasaidia kudhibiti changamoto ya marubani wa nje kutumia Tanzania kama sehemu ya kuongeza masaa ya kuruka kabla ya kuhamia mashirika makubwa ya ndege. 

 

Dkt. Mgaya amesisitiza kuwa kuanzishwa kwa kozi hiyo ni hatua muhimu katika kuimarisha sekta ya usafiri wa anga nchini.




Post a Comment

0 Comments