MIRADI MIKUBWA KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI DAR ES SALAAM

 


📌BAHATI MASANJILA


SERIKALI ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maji ili kuhakikisha wakazi wa Dar es Salaam wanapata huduma bora na ya uhakika ambapo  miradi kadhaa imeanzishwa na mingine inaendelea kukamilika, lengo likiwa ni kuongeza upatikanaji wa maji safi katika jiji hilo lenye wakazi wengi.

Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama Bwire, amesema kuwa juhudi kubwa zinaendelea kufanyika ili kupanua huduma za maji kwa wananchi. 

 

Miongoni mwa miradi inayotekelezwa ni ule wa Mkuranga Awamu ya Pili, unaolenga kusambaza maji katika maeneo kama Dundani, Mwanambaya, Kisemvule, Vikindu, Mwandege, na Kipara Mpakani.

 

Miradi mingine inayolenga kuboresha hali ya upatikanaji wa maji ni ule wa Kazimzumbwi, ambao utahudumia wakazi wa Kifuru, Msimbu, Homboza, Kitanga, na maeneo mengine yaliyo pembezoni mwa jiji.

 

Amesema Pia, Mradi wa Mama Samia Industrial Park unaendelea kutekelezwa ili kuhakikisha maeneo ya Disunyara, Kilangalanga, Kisabi, Mhande, na Mlandizi yanapata maji safi ya uhakika. 

 

Ameongeza kuwa Kwa sasa huduma ya maji safi jijini Dar es Salaam imefikia asilimia 45, huku mipango ya muda mfupi na mrefu ikiwa ni kupanua mtandao wa maji ili kuwafikia wakazi wengi zaidi.

 

Mbali na huduma za maji safi, mamlaka hiyo pia inatekeleza miradi mbalimbali ya majitaka ili kuhakikisha mazingira yanabaki safi na salama kwa wakazi wa jiji hilo. 

 

Kwa mujibu wa Mhandisi Bwire, miradi kadhaa ya usafi wa mazingira imekamilika, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vyoo vya umma katika wilaya zote za Dar es Salaam, hatua inayolenga kupunguza uchafuzi wa mazingira.

 

Aidha, miradi mikubwa ya kuchakata majitaka inaendelea, ikiwemo ule wa Mbezi Beach, unaohusisha ulazaji wa bomba la kilomita 101 kwa gharama ya Shilingi bilioni 132.2. 

 

Amesema Utekelezaji wa mfumo wa majitaka katika maeneo ya Mbezi Juu, Mbezi Chini, Kilongawima, na Salasala tayari umefikia asilimia 57.25, huku ukitarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba 2026.

 

Katika kipindi cha miaka minne iliyopita, DAWASA imefanikiwa kutekeleza miradi 25 yenye thamani ya Shilingi bilioni 987.6. Kati ya miradi hiyo, ile ya thamani ya Shilingi bilioni 232.9 tayari inatoa huduma kwa wananchi, huku mingine yenye thamani ya Shilingi bilioni 754.7 ikiwa katika hatua mbalimbali za utekelezaji.

 

Mhandisi Bwire amesema kuwa mamlaka hiyo pia imeanza utekelezaji wa bwawa la Kidunda kwa gharama ya Shilingi bilioni 335.9, ambalo litaongeza upatikanaji wa maji kwa wakazi wa Dar es Salaam. Hadi sasa, zaidi ya Shilingi bilioni 85.4 zimetolewa kwa ajili ya mradi huo, na ujenzi wake umefikia asilimia 28.

 

Serikali pia imeidhinisha maandalizi ya mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka Mto Rufiji, ambao utahakikisha mahitaji ya maji jijini Dar es Salaam yanatosheleza hadi mwaka 2050. 

 

Kwa mujibu wa Mhandisi Bwire, hatua ya kuandaa michoro ya mwisho na nyaraka za manunuzi ya mradi huo tayari imefikia asilimia 89.

 


Post a Comment

0 Comments