BILIONI 520 KUBORESHA HUDUMA ZA MAJISAFI NA MAJITAKA ARUSHA

 


📌BAHATI MSANJILA

Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jiji la Arusha (AUWSA), Mhandisi Justine Rujomba, amesema mamlaka hiyo imeendelea kuboresha upatikanaji wa majisafi na huduma za majitaka kupitia miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Akizungumza jijini Dodoma katika Ofisi za Idara ya Habari - MAELEZO kuhusu mafanikio ya AUWSA katika miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita, Mhandisi Rujomba amesema mradi mkubwa wa maji wenye thamani ya Shilingi bilioni 520 umekamilika kwa lengo la kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira kwa wakazi wa Arusha.

Aidha, amesema mradi wa majisafi wa Oldonyosambu unaogharimu Shilingi bilioni 6.3, ambao utahudumia wakazi wapatao 29,449 katika vijiji vya Oldonyosambu, Lemanda, Lemong’o, Oldonyowasi na Lesinoni, umefikia asilimia 50 ya utekelezaji.

Katika juhudi za kupanua huduma za maji, AUWSA pia inatekeleza mradi wa kuboresha usambazaji wa maji katika Kata za Baraa, Moivaro, na Moshono kwa kujenga mtandao mpya kutoka visima vya Shangarai hadi tanki la majisafi Moshono One. 

Mradi huu unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji kwa lita milioni 5 kwa siku.

Kwa mwaka wa fedha 2024/25, upatikanaji wa majisafi jijini Arusha umefikia asilimia 99 kupitia mradi mkubwa wa usambazaji maji, ikiwa ni sehemu ya dhamira ya serikali ya kuhakikisha wakazi wa mijini wanapata maji safi na salama kwa asilimia 95 ifikapo 2025.

Mhandisi Rujomba amebainisha kuwa AUWSA imejipanga kuendelea kutekeleza miradi kwa ufanisi na kushirikiana na serikali pamoja na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha huduma za majisafi na usafi wa mazingira zinaboreshwa kwa maendeleo endelevu ya Jiji la Arusha na maeneo ya jirani.




Post a Comment

0 Comments