TPA YATEKELEZA MIRADI 10 YA KIMKAKATI YA BANDARI

 





📌BAHATI MSANJILA


Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) inatekeleza miradi 10 ya kimkakati, ikiwemo ujenzi wa Bandari mpya ya Mbegani wilayani Bagamoyo, utakaogharimu Dola za Kimarekani bilioni 1.5. Miradi hii inalenga kuboresha miundombinu na kuongeza ufanisi wa bandari nchini.

 

Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Plasduce Mbossa, amesema miradi hiyo inatekelezwa chini ya Mpango Kabambe wa Maendeleo ya Bandari (2020–2045) na Programu ya Uboreshaji na Uendeshaji wa Bandari, iliyosajiliwa mwaka 2023 kwa namba ya mradi 4,300.

 

Amesema ushirikishwaji wa sekta binafsi umeongeza ufanisi, ambapo mapato yamepanda kutoka wastani wa Shilingi bilioni 850 kwa mwezi mwaka 2023/24 hadi Shilingi trilioni 1 kwa mwezi mwaka 2024/25.

 

Kwa mujibu wa TPA, kiasi cha shehena kinachohudumiwa kimeongezeka kwa wastani wa asilimia 15.23 kwa mwaka, kutoka tani milioni 20.78 mwaka wa fedha 2021/22 hadi tani milioni 27.55 mwaka wa fedha 2023/24.

 

Vile vile ametaja miradi mingine kuwa ni Ujenzi wa kituo cha reli na mtandao wake ndani ya bandari ya Dar es Salaam na unagharimu dola za kimarekani million 119.955 ambao umelenga kupunguza kiwango cha asilimia 98 cha shehena inayotoka bandarini na ujenzi wa bandari maalum ya kisiwa - mgao mkoani Mtwara kwa ajili ya kuhudumia shehena chafu na utagharimu dola za kimarekani million 171.

 

Amesema mradi huo umelenga kuepusha athari za kimazingira na kuondoa changamoto zinazotokana na kuhudumia mizigo hiyo katika bandari ya Mtwara.

 

Mbossa pia ametaja miradi mingine kuwa ni Ujenzi wa gati namba 12 hadi 15 utakao gharimu dola za kimarekani million 591.564 unaolenga kuongeza ufanisi wa bandari ya DSM na ujenzi wa bandari mpya ya Mbegani Bagamoyo utakao gharimu dola za kimarekani billion 1.5.

 

Amesema miradi hiyo ya kimkakati itakapokamilika italeta manufaa mbalimbali ikiwemo mchango katika Makusanyo ya Mapato ya Nchi.

 

Kadhalika amesema,Mamlaka hiyo imekuwa na mchango katika Ajira Nchini ambapo sekta hiyo huchangia katika kutoa ajira za moja kwa moja kwa kuwa Taasisi za umma na Binafsi zinazofanya kazi Bandarini zimeajiri watumishi wanaotoa huduma Bandarini.

 

Aidha, katika mwaka wa fedha wa 2022/23 mchango wa sekta ya bandari ulikuwa Shilingi trilioni 10.8 sawa na asilimia 7.3 ya pato la Taifa lililokuwa Shilingi trilioni 148.3.

 

TPA inasimamia bandari rasmi 131 zilizoko Bahari ya Hindi na Maziwa Makuu, ikiwa na majukumu makuu kama kuendeleza bandari, kushirikisha sekta binafsi, na kusimamia uendeshaji wa shughuli za bandari.















 


Post a Comment

0 Comments