MITI MILIONI 686.24 YASTAWI KATI YA MILIONI 866.7 ILIYOPANDWA NCHINI

 


📌BAHATI MSANJILA

Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Khamis Hamza Khamis, amesema kuwa jumla ya miti milioni 686.24 iliyopandwa katika halmashauri mbalimbali nchini imestawi, sawa na asilimia 82.3 ya miti yote milioni 866.7 iliyopandwa kati ya mwaka 2020/2021 hadi 2023/2024.

Mhe. Khamis ametoa taarifa hiyo Februari 5, 2025, bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Mhe. Tunza Malapo alietaka kufahamu iwapo tathmini imefanyika ili kubaini miti inayopandwa, kutunzwa, na kukua kama sehemu ya juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Ameeleza kuwa tathmini ya upandaji wa miti hufanyika kila mwaka kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI ili kupambana na uharibifu wa ardhi, ukame, na kuenea kwa hali ya jangwa hivyo Kwa msimu wa mwaka 2024/2025, tathmini inaendelea kufanyika ili kubaini idadi ya miti iliyopandwa na iliyostawi kote nchini.

Aidha, Mhe. Khamis amesisitiza umuhimu wa kushirikisha wananchi na sekta binafsi katika kampeni za upandaji wa miti ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kutunza mazingira.

Ametoa wito kwa Watanzania kutumia mvua zinazonyesha kipindi hiki kupanda miti katika maeneo mbalimbali.

Akijibu swali la nyongeza la Mhe. Tunza Malapo kuhusu mkakati wa kuhakikisha miti inatunzwa, Mhe. Khamis amesema kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais ina maafisa viungo katika mikoa yote ya Tanzania Bara wanaosimamia na kufuatilia utekelezaji wa zoezi la upandaji miti.

Vilevile, ameeleza kuwa kampeni mbalimbali zimeanzishwa ili kuhamasisha upandaji wa miti katika vyanzo vya maji, mashuleni, na pia matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kupunguza ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

Post a Comment

0 Comments