MAJAJI, MAHAKIMU TEKELEZENI WAJIBU WENU KWA HAKI MSISIJIFANANISHE NA MIUNGU

 

       


📌BAHATI MSANJILA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka majaji na mahakimu kuhakikisha wanatekeleza wajibu wao kwa haki, kwa kuzingatia makubaliano ya kisheria na kikatiba, badala ya kujiona kama miungu watu.

 

Rais Samia ameyasema hayo Februari 3, 2025, wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini, yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo inadhihirisha dhamira ya kuifanya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kuwa na mipango madhubuti ya kukuza haki nchini.

 

Ameeleza kuwa utekelezaji wa dira hiyo hautakuwa rahisi, hivyo ni muhimu kwa Mahakama na wadau wake kuanza kujipanga kwa umakini ili kuhakikisha haki inapatikana kwa ufanisi zaidi.

 

Akizungumzia usimamizi wa haki jinai na haki madai amesema kuwa kaulimbiu ya mwaka huu isemayo Tanzania ya 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo.”  inampa faraja kwa sababu inadhihirisha kuwa agizo lake alilolitoa kuhusu uboreshaji wa taasisi za haki jinai linaendelea kufanyiwa kazi.

 

Aidha, amesema kuwa Serikali imeendelea kuiwezesha Tume ya Utumishi wa Mahakama kutekeleza majukumu yake ipasavyo. 

 

Amebainisha kuwa serikali inatambua kuwa katika kazi kuna haki na wajibu, na ndiyo maana imekuwa ikisisitiza wajibu wa mahakama na taasisi za haki jinai na haki madai katika kuimarisha ustawi wa jamii na haki nchini.

 

Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma, amesema kuwa maadhimisho haya hutumika kuwaombea watoa haki na kuwakumbusha kuwa kazi yao ni utume wa Mungu, hivyo wanapaswa kutenda haki kwa uadilifu.

 

Ameeleza kuwa wananchi waliopata elimu hiyo wamewasilisha maoni mbalimbali, ambayo ni mtaji muhimu wa kujipima, kujitathmini, na kuweka mikakati thabiti ya kuboresha huduma za utoaji haki.

 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari, amesema kuwa ofisi yake inaamini kuwa kupitia ushirikiano wa wananchi na taasisi husika, mafanikio makubwa yatafikiwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kwa usawa.

 

Ameongeza kuwa mfumo wa haki utakuwa nguzo muhimu katika kufanikisha Tanzania yenye misingi imara ya haki na usawa, kwa mujibu wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Boniface Mwakabusi, amesema kuwa ushirikiano kati ya chama hicho na Serikali si dalili ya kupewa upendeleo, bali ni utekelezaji wa wajibu wa pamoja wa kuhudumia wananchi.

 

Ameishukuru Wizara ya Katiba na Sheria kwa kuwapatia gari litakalowasaidia kuwafikia wananchi kwa urahisi. Amesema kuwa TLS ipo tayari kupokea msaada wowote kutoka kwa mtu au taasisi yoyote kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa huduma za kisheria kwa wananchi.

 

Maadhimisho ya Siku ya Sheria ni tukio muhimu linalotoa fursa kwa wadau wa sekta ya sheria kujadili changamoto na mafanikio katika mfumo wa utoaji wa haki nchini.

 

Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini Tanzania kwa mwaka 2025 ni: “Tanzania ya 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo.” 

 










Post a Comment

0 Comments