MAGARI 150 YA ZIMAMOTO KUBORESHA HUDUMA ZA UOKOAJI NCHI NZIMA

 


  📌BAHATI MSANJILA

Serikali inaendelea kuimarisha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kuliwezesha kwa vitendea kazi muhimu, ikiwemo ununuzi wa magari 150 ya kisasa ya kuzima moto na uokoaji, pamoja na vifaa vingine vinavyohitajika.


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Innocent Bashungwa,amebainisha hayo tarehe 3 Februari 2025 alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Ngorongoro, Emmanuel Shangai, aliyetaka kufahamu lini Serikali itanunua gari la zimamoto kwa ajili ya Wilaya ya Ngorongoro.

“Kwa sasa, Serikali inatekeleza mradi wa ununuzi wa vifaa mbalimbali vya kuzima moto na uokoaji, ikiwemo magari 150 ya zimamoto ambayo yatakapowasili nchini, yatasambazwa kote nchini, ikiwemo Wilaya ya Ngorongoro,” amesema Bashungwa.

Aidha, Waziri huyo amefafanua kuwa Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari imewezesha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kupata magari 12 ya kisasa, ambapo moja lilitumiwa kwa mafanikio kuzima moto katika jengo la TRA Kariakoo.

Mbali na hilo, Bashungwa amebainisha kuwa Serikali ina mpango wa kununua helikopta maalum kwa ajili ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ili kuongeza ufanisi katika operesheni za uokoaji na kudhibiti majanga ya moto.

Pamoja na hilo, maafisa, wakaguzi na askari wa jeshi hilo wataendelea kupatiwa mafunzo maalum ili kuongeza ujuzi wao katika kukabiliana na dharura.

Hatua hizi ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linakuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi katika kukabiliana na majanga ya moto na uokoaji wa wananchi kote nchini.





Post a Comment

0 Comments