CCM YASISITIZA USHINDI KWA UADILIFU, SIFA ZA WAGOMBEA KUPIMWA KWA VIGEZO MADHUBUTI

 



📌BAHATI MSANJILA

Chama cha Mapinduzi (CCM) kimekemea  tabia ya baadhi ya wanachama wa Chama hicho  wakiwemo Wabunge kuanza kufanya kampeni  chafu  zenye nia ya kuchafuana wenyewe kwa wenyewe kabla  ya uchaguzi nakusisitiza kuwa wagombea watapimwa kwa sifa, tabia na uwezo wa kukubalika katika jamii badala ya nguvu ya fedha.

Katibu Mkuu wa CCM na mgombea mwenza wa kiti cha urais, Dkt. Emmanuel Nchimbi amekemea tabia hiyo leo jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya Watendaji wa Kata na Makatibu wa Matawi Mkoa wa Dodoma, amesisitiza kuwa mfumo mpya wa upigaji kura umeongeza idadi ya wapiga kura kwa asilimia 900 ili kuondoa rushwa na kupima wagombea kwa maendeleo badala ya fedha.

Katika hotuba yake, Dkt. Nchimbi amesisitiza kuwa ushindi wa chama unatokana na uimara wake, utendaji wa viongozi, na utekelezaji wa ilani ya chama.

 Amesema chama kinapaswa kujengwa kwa misingi ya uadilifu na si kwa kuzingatia kiwango cha fedha cha mgombea.

 Kwa mujibu wake, kabla ya mgombea kupitishwa, atapimwa kwa sifa, tabia, na uwezo wa kukubalika katika jamii, Dkt. Nchimbi ameonya kuwa ni kosa kubwa la kimaadili kupuuza Katiba na kanuni za chama.

Amesema baadhi ya watu wamekuwa wakipitisha fomu kwa wanachama na viongozi kwa njia zisizo halali ili mgombea apitishwe bila kupingwa Amewataka waache mara moja tabia hiyo, akisisitiza kuwa yeyote atakayebainika ataondolewa kwenye orodha ya wagombea.

Aidha, amebainisha kuwa wanachama wote wana haki ya kugombea nafasi za uongozi, na kwamba juhudi zozote za kuwashawishi wajumbe waache kupinga mgombea fulani zitapelekea wahusika kuenguliwa.

Katibu Mkuu huyo pia ameonya kuhusu tabia ya wanachama kufanya shughuli za kifamilia na kualika wajumbe kwa malipo ili kupata kura. Amesema taarifa za watu wa aina hiyo zipo na hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.

Amesema Rushwa imepata jeraha la kudumu kutokana na mfumo huu, na wanachama pamoja na wagombea wachapakazi wamefurahi kwa kuwa wanapata nafasi ya kutumikia wananchi.

Kwa upande wake, Katibu wa CCM Mkoa wa Dodoma Pili Agustino amesema mafunzo haya ni sehemu ya utekelezaji wa ilani ya chama na yatawasaidia watendaji wa kata na makatibu wa matawi kufanya kazi yao kwa ufanisi zaidi.

Naye Katibu wa NEC Organization Issa Gavu, amesema mafunzo haya ni muendelezo wa maelekezo ya Mwenyekiti wa CCM, yakisisitiza kuwa chama huanzia mashinani, ambako ndiko kuna wanachama na wapiga kura. Amewataka washiriki wa mafunzo hayo kuyazingatia kwa umakini ili yawe na manufaa makubwa kwa chama na jamii kwa ujumla.

Jumla ya washiriki 274 wanahudhuria mafunzo haya, wakitarajiwa kuimarisha uongozi wa chama katika ngazi za kata na matawi ili kuhakikisha ushindi wa CCM unapatikana kwa misingi ya uadilifu, ushawishi na maendeleo.














Post a Comment

0 Comments