BODI YA WMA YAMTAKA MKANDARASI KUKABIDHI JENGO FEBRUARI 10

 


📌BAHATI MSANJILA

Wajumbe wa Bodi ya Wakala wa Vipimo (WMA) wametembelea jengo jipya la Makao Makuu ya wakala huo na kumwagiza mkandarasi kuhakikisha anakamilisha kazi na kukabidhi rasmi jengo hilo ifikapo Februari 10 mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukagua hatua za ujenzi wa jengo hilo Mwenyekiti wa Bodi ya WMA Prof. Eliza Mwakasungura, amesema wajumbe wa Bodi wameridhishwa na maendeleo ya ujenzi baada ya kukagua jengo hilo lenye ghorofa tano huku wakielekeza marekebisho madogo yaliyosalia, kama upakaji rangi, yakamilike kabla ya tarehe ya makabidhiano.

“Nimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutenga Shilingi bilioni 6.2 kwa ajili ya ujenzi huu. Pia, nampongeza Waziri wa Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Jafo, pamoja na menejimenti yake kwa usimamizi mzuri wa mradi huu,” alisema Prof. Mwakasungura.

Kwa upande wake,Mtendaji Mkuu wa WMA,Alban Kihulla amesema ujenzi wa jengo hilo umefikia asilimia 97 na tayari mkandarasi amepewa fedha yote Sh bilioni 6.2.

“Tuna hakika kazi iliyobaki itakamilika kwa wakati. Kukamilika kwa jengo hili kutasaidia kutatua changamoto ya majengo kwa Makao Makuu na Ofisi ya Mkoa, kwani sasa wote watakuwa hapa,” alisema Kihulla.

Kwa upande wake, Mkandarasi wa jengo hilo, Mohammed Jafferji wa kampuni ya Mohammed Builders, amethibitisha kuwa kazi inaendelea na wanajitahidi kuhakikisha wanakabidhi jengo hilo kwa muda uliopangwa.

“Kufikia Februari 10 tunatarajia kuwa tumemaliza kazi zote zilizobaki, tukishirikiana na mshauri elekezi ili kuhakikisha kila kitu kipo sawa,” alisema Jafferji.

Jengo hili jipya linatarajiwa kuboresha mazingira ya kazi kwa Wakala wa Vipimo na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma zake.







 


Post a Comment

0 Comments