SERIKALI YATOA UFAFANUZI GHARAMA ZA KUUNGANISHA UMEME VIJIJINI

 


📌BAHATI  MSANJILA


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga, kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, ametoa ufafanuzi kuhusu gharama za kuunganishiwa umeme maeneo ya vijijini, akieleza kuwa wananchi wa vijijini wanapaswa kulipia shilingi 27,000/-, huku wale wa vijiji mji wakitakiwa kulipa shilingi 320,960/-.

 

Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Januari 30, 2024, bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Bukene, Mhe. Selemani Zedi, aliyetaka kufahamu kwa nini wakazi wa Bukene na Itobo hawaunganishiwi umeme kwa gharama ya shilingi 27,000/-.

 

Mheshimiwa Spika, maeneo ya Bukene na Itobo ni vijiji mji, hivyo gharama ya kuunganisha umeme inakuwa shilingi 320,960/- kwa mujibu wa utaratibu wa serikali,” amesema Mhe. Kapinga.

 

Amebainisha kuwa serikali inaendelea kufanya tathmini kuona kama kuna uwezekano wa kuboresha gharama hizo kulingana na tathmini zilizofanyika. Pia, ameeleza kuwa amemuagiza Meneja wa Mkoa wa Tabora na Meneja wa Wilaya ya Nzega kufanya tathmini ya kina ili kupata majibu sahihi kuhusu maeneo hayo na kuondoa mkanganyiko uliopo.

 

Katika hatua nyingine, akijibu swali la Mbunge wa Kilombero, Mhe. Abubakari Asenga, kuhusu kwa nini wakazi wa Katinduka wanalipia shilingi 320,960/- licha ya kuwa kijijini, Mhe. Kapinga amesema gharama ya shilingi 27,000/- inahusu maeneo yaliyotambuliwa rasmi kama vijiji na ambayo yamepata ufadhili wa miradi ya umeme vijijini. Ameeleza kuwa siyo kila eneo linakidhi vigezo hivyo, na kwamba Katinduka ni sehemu ya mtaa, hivyo gharama yake ni tofauti.


Kwa upande mwingine, Mhe. Kapinga amejibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Anatropia Theonest, kuhusu upatikanaji wa umeme katika vijiji vya Buganza na Nyarigongo wilayani Kyerwa. Amesema umeme umeshafika katika makao makuu ya vijiji hivyo, na kwamba mkandarasi anaendelea na kazi ya kusambaza umeme katika kilometa mbili za ziada ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

 

Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa wananchi kufahamu tofauti ya maeneo ya vijiji na vijiji mji ili kuepusha mkanganyiko kuhusu gharama za kuunganishiwa umeme, huku ikiahidi kuendelea kufanya maboresho kulingana na tathmini zinazoendelea kufanyika.

 



Post a Comment

0 Comments