SERIKALI YAPIGA JEKI HUDUMA ZA AFYA YA UZAZI KUPAMBANA NA UTOAJI MIMBA USIO SALAMA

 


📌BAHATI MSANJILA

Takwimu za Serikali kwa mwaka 2024 zinaonyesha kuwa idadi kubwa ya wanawake na wasichana wameathirika kutokana na utoaji mimba usio salama, ambapo 181,071 walihitaji huduma katika vituo vya afya na kuhudumiwa kama wagonjwa wa nje, huku 32,512 walilazwa hospitalini kwa ajili ya matibabu zaidi kutokana na matatizo ya kuharibika kwa mimba.

Aidha, takwimu zinaonesha kuwa kati ya mwaka 2022 hadi 2024, wanawake 92 walipoteza maisha kutokana na matatizo mbalimbali yaliyosababishwa na kuharibika kwa mimba.

Akijibu swali la Mhe. Fatma Hassan Toufiq Mbunge Viti Maalum) Leo Bungeni Jijini Dodoma Naibu Waziri wa Afya mhe. Godwin Mollel ameeleza kuwa changamoto za utoaji mimba usio salama zinaathiri afya ya wanawake na wasichana, na kwamba Serikali inatambua umuhimu wa kutoa huduma bora za afya ya uzazi.

Ameeleza kuwa katika juhudi za kupunguza athari za utoaji mimba usio salama, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya ya uzazi na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu hatari zinazohusiana na utoaji mimba katika mazingira yasiyo salama.

Waziri huyo amesisitiza kuwa takwimu hizi zinapaswa kuchukuliwa kama kengele ya tahadhari kwa jamii na Serikali, ili kuhamasisha watu kuchukua hatua za tahadhari na kufuata mifumo sahihi ya uzazi, ikiwa ni pamoja na kutafuta huduma bora za afya wakati wa matatizo ya uzazi.

Serikali pia inaendelea kutoa maelekezo kwa vituo vya afya kuhusu utoaji wa huduma za dharura na kutoa elimu ya afya kwa jamii ili kupunguza idadi ya vifo vinavyotokana na utoaji mimba usio salama.

Katika mwaka 2022, Serikali ilitangaza kuwa inasimamia kwa karibu utekelezaji wa sera na mipango ya afya ya uzazi, ikiwa ni pamoja na kutoa huduma kwa wanawake na wasichana walioathirika na utoaji mimba Hata hivyo bado kuna changamoto kubwa ya wanawake wengi kutafuta huduma hizi kwa kuchelewa, jambo linaloathiri matokeo ya afya yao.

Serikali imesisitiza kuwa, licha ya changamoto hizo, itaendelea kutekeleza mikakati ya kupunguza athari za utoaji mimba usio salama, ikiwa ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa huduma za afya ya uzazi na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa huduma za afya ya uzazi.




Post a Comment

0 Comments