SERIKALI YA ZANZIBAR YASISITIZWA KUJENGA MFUMO IMARA WA UNUNUZI WA UMMA

 


📌BAHATI MSANJILA

NAIBU Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande, ameishauri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuweka mfumo madhubuti wa ununuzi wa umma kwa kutumia wataalam wa ndani, akisisitiza umuhimu wa kusimamia kwa ufanisi fedha za Serikali zinazotumika katika ununuzi.

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa mazungumzo na Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, iliyotembelea Mamlaka ya Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa lengo la kujifunza masuala ya ununuzi, Mhe. Chande alisema kuwa mfumo bora wa ununuzi siyo tu utarahisisha michakato, bali pia utaongeza uwazi na kuhakikisha thamani halisi ya fedha inapatikana.

“Zaidi ya asilimia 70 ya bajeti zetu hutumika kwenye ununuzi wa umma. Kwa hiyo, tunapojadili Muswada wa Sheria ya Ununuzi, ni lazima tuhakikishe sheria inakuwa thabiti ili kuondoa changamoto zinazoweza kujitokeza,” alisisitiza Mhe. Chande.

Aidha, aliipongeza Kamati hiyo kwa kuchukua hatua ya kuja kujifunza katika PPRA kabla ya kupitisha Muswada wa Sheria ya Ununuzi wa Umma unaotarajiwa kujadiliwa katika Baraza la Wawakilishi Zanzibar. Pia, aliwataka kuendelea kushirikiana na PPRA kwa kutembelea mifumo iliyoimarika, ikiwemo mfumo wa ununuzi uliowekwa jijini Arusha.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mhe. Mwanaasha Khamis Juma, alisema kuwa hatua ya kuja kujifunza ni muhimu kwa kuwa kamati hiyo inawajibika kuhakikisha fedha za Serikali zinatumika kwa tija.

“Kamati yetu inahusika moja kwa moja na kupitisha bajeti ya Serikali ambayo ndani yake kuna miradi mikubwa. Tumekuja kujifunza kutoka kwa wenzetu wa PPRA kuhusu sheria, taratibu na changamoto zinazohusu ununuzi.




 


Post a Comment

0 Comments