KIKWETE AWAAGIZA WAKURUGENZI KUSIMAMIA MAPATO NA KULIPA MISHAHARA KWA WAKATI

 ðŸ“ŒRHODA SIMBA

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Ajira, Vijana na Watu Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete amewaagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri nchini kusimamia mapato ili kulipa mishahara na malimbikizo ya madai kwa watumishi ikiwemo fedha za likizo.

Kadhalika amewataka wakurugenzi kulipa posho za watumishi wa kada mbalimbali ikiwemo watendaji wa Kata.

Kikwete ameyasema hayo leo Januari 15,2025 jijini Dodoma wakati akifungua kikao cha 30 cha Baraza kuu la Chama cha wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU)

Amesema Serikali haitawafumbia macho waajiri ambao hawatekelezi takwa la kisheria ikiwemo kuhuisha mabaraza ya wafanyakazi, na kwamba Serikali imesikia na kuelewa changamoto zote zilizoanishwa na ipo tayari kufanyia kazi.

Awali akisoma Risala Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) Katibu wa Chama hicho Rashid Mtima, amebainisha changamoto mbalimbali wanazokutana nazo watumishi wa umma ikiwemo fedha za likizo kutolipwa kwa wakati, Malipo ya Leseni kwa Kada ya Afya,Fedha za Uhamisho Kutolipwa, pamoja na Changamoto za Mfumo wa PEPMIS.

Akizungumzia kuhusu mfumo wa kupima utendaji kazi wa watumishi wa umma (PEPMIS) Mtima amesema umekumbwa na changamoto za mtandao na ukosefu wa mafunzo kwa watumishi waliopo maeneo ya vijijini, hali inayozuia utekelezaji bora wa mfumo huo.

Pia, Mtima alikumbusha kuwa baadhi ya halmashauri hazijahuisha mabaraza ya wafanyakazi kama inavyotakiwa kisheria. Hadi sasa, Halmashauri 41 kati ya 185 hazijafanya hivyo, jambo linalozuia utatuzi wa changamoto za watumishi kwa wakati.

Hata hivyo, TALGWU ilipongeza juhudi za Serikali ya awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha utumishi wa umma. Miongoni mwa hatua zilizotajwa ni pamoja na kupandisha madaraja ya watumishi, kuboresha mifumo ya kikokotoo cha mafao, na kuimarisha miundombinu ya usafiri, ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa mradi wa treni ya umeme (SGR).

Kikao hicho kimehitimishwa kwa wito wa mshikamano miongoni mwa wanachama wa TALGWU na Serikali ili kuhakikisha changamoto zilizotajwa zinafanyiwa kazi kwa manufaa ya wafanyakazi na maendeleo yao.




Post a Comment

0 Comments